Vikao na Kazi za Vikundi, Vikoba

Mambo 10 Muhimu Vinavyotakiwa Kuimarisha Kikundi

Utangulizi

Makala haya yamelenga katika kusaidia vikundi vidogo vidogo vya aina tofauti kuanzia zile za kiuchumi, kijamii, kielimu, kitaaluma, kidini na kikabila nk. Ni matumaini yangu kuwa makala hii haitatumiwa kama muwa arobaini wa kumaliza matatizo ya kwenye vikundi bali itatumika kama chachu ya kuwa mbunifu zaidi kwenye kuhakikisha vikundi vinakuwa na matatizo ambazo zinaweza ama kuzimudu au kuziondoa kabisa.

Kwa nini ninasisitiza matatizo, kwa sababu matatizo ndizo zinazouwa vikundi vingi na matatizo mengi yanatengenezwa na watu kwa kukusudia au kutojua. Lakini pia matatizo huimarisha vikundi kama hayo matatizo yatachukuliwa kama fursa ya kufanya vizuri zaidi.

Kikundi ni nini?

Kikundi ni muungano wa watu wawili au zaidi wenye lengo kufanikisha mradi wa kutatua matatizo yanayowakabili kama vile matatizo ya kiuchumi, kijamii, kisiasa, kikabila, kielimu nk.

Aina za Vikundi

Yafuatayo ni aina za vikundi ambavyo vipo na vinatumika kutatua matatizo mbalimbali zinazowakabili watu/jamii

Jina la kikundi Sekta Lengo Aina ya watu/washiriki
Kikoba Uchumi Kukopeshana Watu wa aina zote
Succos Uchumi Kukopeshana Watu wa aina zote
Kibati Uchumi Kukopeshana Watu wa aina zote
Vyama  vya Makabila Jamii Kujaliana Kabila husika
Shule/Vyuo Elimu Kusaidiana katika masomo Wanafunzi
Vyama vya kisiasa Siasa Kuongoza jamii kisiasa Wanasiasa
Vyama vya kitaaluma Taaluma husika Kusaidiana kitaaluma Wanataaluma kama wahandisi, waalimu, madaktari, wanasheria nk
Vyama na klabu za michezo Michezo Kusaidia kukuza michezo, Kushiriki kucheza pamoja, kushinda mataji nk Wanamichezo
Vyama vya burudani Burudani Kusaidia kukuza wasanii, na usanii  nk Wasanii

Kwa nini vikundi?

  1. Kikundi ndio njia pekee ya kulifanya tatizo kuwa dogo na rahisi kulimudu au kulitatua.
  2. Kwenye vikundi mtu anatiwa hamasa kwamba kumbe anaweza
  3. Kwenye vikundi mtu anajifunza pia nidhamu
  4. Kwenye vikundi hasa zile za kiuchumi mtu anajifunza kuweka akiba kwa ajili ya maendeleo yake

Mambo 10 Muhimu ya Kuzingatia ili Vikundi Viimarike

  1. Kuwa na katiba ya kikundi
  2. Kuchagua viongozi bora wenye kuweza kutetea katiba
  3. Kuweka sheria ndogondogo (katiba itoe mwongozo wa namna nzuri ya kuweka, kupitisha na kuboresha hizo sheria ndogondogo)
  4. Kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za kikundi
  5. Kujenga urafiki na wenzako wa kikundi nje ya kikundi
  6. Kuepuka Kansa kuu 4 za kuua vikundi
    1. Kukosoa wengine,
    2. kulaumu wengine
    3. kushindana na kujiona wa maana kuliko wengine
    4. kujilinganisha na mwingine
  7. Kufikiria  wini/win kwa kila jambo, wewe upate haki yako na mwenzako katika kikundi pia apate haki yake
  8. Kujifunza na kujenga tabia ya kuwasikiliza wengine na kuwaelewa kabla ya kuchangia
  9. Kuepuka tabia za wanyama zenye kuua umoja
  10. Kufanya tathmini na maboresho ya mahusiano kila baada ya mwaka

1.      Kuwa na katiba ya kikundi

Katiba ambayo ni rahisi kueleweka na imebeba mambo ya msingi ni lazima iwepo ili iwe mwongozo wa sheria zote na kanuni zote za kikundi. Katiba ni vyema ikaandaliwa na mtaalamu mwenye uzoefu na kuandaa katiba za vikundi. Katiba ikiwa nzuri kikundi kitasalimika kwa muda mrefu lakini katiba ikiwa mbovu itawagombanisha wanachama na kikundi kinaweza kufa ndani ya muda mfupi

2.      Kuchagua viongozi bora wenye kuweza kutetea katiba

Viongozi wachaguliwe kwa uwezo wao wa kusimamia katiba na sheria zilizowekwa na pia wawe wa kwanza kufuata kila kipengele cha sheria, kanuni na taratibu. Watu wanaoongozwa kwa asili wanaangalia viongozi wao wanafanya nini, tabia zao na wao wanakopy na kupaste. Mfano kiongozi akiwa na tabia ya kuchukua mkopo na asirudishe kwa wakati, na wao wakichukua mkopo hawatarudisha kwa wakati, mfano mwingine, kama kiongozi ana tabia ya kuchelewa kikao na wanachama watajenga hiyo tabia ya kuchelewa vikao.

3.      Kuweka sheria ndogondogo

Kuwepo na sheria na kanuni ndogo ndogo ambazo zitakuwa zikiboreshwa mara kwa mara kulingana na uhitaji na muda ili kuipa afya kikundi. Katiba itoe mwongozo wa namna nzuri ya kuweka, kupitisha na kuboresha hizo sheria na kanuni ndogondogo

4.      Kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za kikundi

Kila mjumbe, mwanachama hata kama ni kiongozi, ni vyema sheria, kanuni na taratibu za kikundi viheshimiwe na kufuatwa . Mmoja wa mwanachama hata kama ni kiongozi akianza kufunja na kukiuka kanuni, taratibu na sheria itatoa mwanya kwa wengine hata wale ambao hawakuwazaga kuvunja sheria kuanza kuvunja. Huko mbeleni itakuwa ni ngumu tena ngumu sana kuwarudisha wanachama ili watii na kufuata sheria na ndio tiketi ya kuua kikundi.

5.      Kujenga urafiki na wenzako wa kikundi nje ya kikundi

Kama wanachama nje ya kikundi ni maadui kwa asilimia kubwa wataendelea kuwa maadui hata kwenye kikundi na kadhalika kama wanachama watakuwa ni marafiki nje ya kikundi kwa asilimia kubwa wataendelea kuwa marafiki ndani ya kikundi. Mfano kama wanachama wanajaliana kwa mambo ya kijamii kama harusi, wanafanya biashara za pamoja, nk watadumisha hiyo zaidi kwenye kikundi. Vikundi vitakuwa na afya sana kama huu urafiki na umoja utaanzia nje yaani kwenye majumba yao, ujirani mwema, makazini, kwenye biashara, makanisani nk.

6.      Kuepuka Kansa kuu 4  za kuua vikundi

Kansa ni ugonjwa mbaya sana, usipowahiwa unaua. Tiba yake ni mionzi au kwa lugha ngumu kuchoma moto. Kansa hapa tunalenga tabia ambazo zisipowahiwa kuchomwa moto zitauwa kikundi.

Tabia hizo ni hizi hapa chini:

  1. Kukosoa wengine,
  2. Kulaumu wengine
  3. Kushindana na wenzako
  4. Kujilinganisha na mwingine

Kukosoa Wengine,

Sio dhambi kukosoa bali tabia ya kukosoa ndio dhambi. Tabia ya kukosoa wengine ni hatari kwani inauwa mchango mzuri kutoka kwa wanachama. Wewe fikiria kila ukichangia kuna mtu anakusubiri ili akuponde, wengi wetu hatuwezi tunaamua kunyamaza tu ili much know yeye peke yake achangie. Badala ya kukosoa unaweza kuchangia kwa kuboresha kile kilichopungua kwenye mchango wa mwenzako bila kupotosha au kupindisha wazo lake la msingi. Au ukatoa wazo mbadala huku ukuainisha wazi madhara kama tukulifuata wazo la mchangiaji wa kwanza. Kama utatoa mawazo tofauti na kulikataa wazo la mwenzako, kwanza omba msamaha na eleza nia yako safi ya kuboresha kikundi na utoe nafasi kwa wajumbe kuafiki au kukataa. Kwa tabia nina maanisha kila mara wewe unafanya hivyo hata kwa yale mawazo mazuri ya wenzako wewe utatafuta cha kukosoa tu.

Kulaumu Wengine

Hii iko wazi, kuna watu wao ikitokea tatizo ni kuwanyooshea wengine vidole na maneno ya kulaumu wengine. Mfano inaweza kuwa alitaka mkopo na wenzako wakaona sio busara kumpa mkopo kama alivyoomba kwa sababu ya wazi kabisa. Lakini yeye badala ya kupokea kwa mtizamo chanya maamuzi ya wenzake, yeye ataanza kusambaza maneno najua mwenyekiti hanipendi, najua fulani yuko karibu na mwenyekiti ndiye chanzo nk.

Hata kama kuna sababu ya kulaumu, kulaumu ni dhambi na itakukula wewe na kikundi chote kinaweza kuangamia kwa sababu ya tabia yako ya kulaumu.

Kushindana na Wenzako

kushindana na kujiona wewe wa maana kuliko wengine inaweza kuongeza chuki na kupunguza mshikamano kwenye kikundi. Wewe fikiria hali ya kushindana ikienea kwa wanakikundi wote, kutatokea nini? Kila mwanakikundi ataanza kujali mambo yake tu na ikawa ndio chimbuko la ubinafsi na hatimaye kuuwa kikundi.

Kujilinganisha na Mwingine

Kujilinganisha na wenzako ni dhambi kubwa kwa sababu kwa asili hatulingani. Hatulingani kiakili, kiuchumi, kiustaarabu, kielimu, kiafya, kimtizamo nk.

Kila mtu Mungu alimuumba kwa utofauti wa kipekee na kwa hiyo wewe ni wewe tu hakuna wa kufanana na wewe na wewe hutaweza kufanana na mwingine katika ulimwengu huu wote.

Kama mwenzako anamiliki gari na wewe huna usianze kucheza rafu ili na wewe uwe na gari kama fulani kwa sabau lazima utatenda dhambi ndipo upate gari kama fulani. Mfano itakubidi utapeli, uibe, urushe nk. Na sehemu ya kutekeleza hayo yote kwa ukaribu na urahisi ni kwenye kikundi.

7.      Kufikiria  Kupata na Mwenzako Apate (Wazungu wanaita Win/win)

Kufikiria  kupata na mwenzako apate kwa kiingereza wanaita “wini/win” kwa kila jambo ni ile hali ya kumtakia mwenzako daima apate haki zake kama wewe unavyopata haki zako. Yeye afanikiwe kama wewe unavyofanikiwa. Yeye apate fursa za kimaendeleo kama wewe unavyopata hizo fursa nk.

Inapokuja kutakiana mema au mabaya, kuna watu wa aina nne kwenye vikundi

  1. Watu wanaopenda wapate na wenzao pia wapate – Win/win – ndio mada ilipo
  2. Watu wanaopenda wao wapate na wenzao wakose – Win/Lose – Wababe/ Wabinafsi
  3. Watu wanaopenda wao wakose na wenzao wapate – Lose/win – Masifa
  4. Watu wanaopenda wao wakose na wenzao wakose – Lose/lose – Maskini jeuri
  5. Watu wanaopenda tofauti zao zisiharibu uhai wa kikundi au mahusiano – win/win – Wastaarabu

Watu wanaopenda wapate na wenzao pia wapate – Win/win

Watu wa kundi hili ndio wanaotakiwa katika kikundi kwa sababu wanapenda haki, kila mwanakikundi apate sawasawa na haki yake

Watu wanaopenda wao wapate na wenzao wakose – Win/Lose

Watu wa kundi hili hawatakiwi kabisa kwa sababu wao ni wabinafsi sana wanataka wao tu wapate haki yao na wenzao wakose

Watu wanaopenda wao wakose na wenzao wapate – Lose/win

Pia watu wa kundi hili hawatakiwi kabisa kwa sababu wao wako tayari wakose ili wenzao wapate. Hawa wanaitwa masifa, ili waonekane wao wanajali wengine sana. Saa nyingine ni janja tu labda wanataka kikubwa zaidi kama kuchaguliwa kuwa viongozi nk. Watu wa namna hii ni rahisi sana baadaye kuja kuwa viongozi wabaya sana kwani watataka kurudisha gharama za wao kupoteza huko nyuma.

Watu wanaopenda wao wakose na wenzao wakose – Lose/lose

Watu hawa ni watu waliokata tamaa. Wanaona dhahiri kuwa hawataweza kupata kitu fulani kwa hiyo wako tayari kuharibu, kuuwa ili na wengine wakose. Katika aina za wanakikundi wote, hawa wa akina lose/lose ndio wabaya kuliko wote kwani wako tayari kikundi kife ili wao wakose na wengine wakose pia. Watu wa aina hii wanaitwa maskini jeuri kwani kwa vile hawana uwezo wa kupata watakacho basi wako tayari kuvuruga, kuua, kukwamisha ili wote wakose

Watu wanaopenda tofauti zao zisiharibu uhai wa kikund – win/win

Watu wa kundi hili ni wale ambao wako tayari kufanya jambo wasilolipenda kwa manufaa ya wote wakiwemo wao. Kwa kimombo wanaita “agree to disagree” yaani kukubalina kutokubaliana.

Hawa pia kama lile kundi la kwanza wanatakiwa sana kwenye kikundi kwa uhai na afya nzuri ya kikundi. Kwanini, kwa sababu kwenye vikundi saa nyingine tunapitisha maamuzi ambayo haiwafurahishi baadhi ya wanakikundi na kwa hiyo japo hawakubaliani na utaratibu huo lakini kama itakuwa na manufaa kwa kikundi wako tayari kukubaliana na jambo wasililitaka. Kundi la watu kama hawa wanaitwa wastaarabu

8.      Kuwasikiliza Wengine

Tabia ya kuwasikiliza na kuwaelewa wengine kabla ya kuchangia au kutoa hukumu ni msingi mzuri sana wa maelewano kwenye kikundi.

Ngoja nikupe mfano wa Nyani na kambare

Siku moja Nyani katika pitapita yake alikutana na Kambare kwenye kibwawa kidogo kilichokuwa na maji kidogo. Huyo Kambare kwa sababu ya maji kidogo alikuwa akitapa-tapa sana kutafuta maji mengi.

Nyani kwa haraka na huruma nyingi kwa yule Kambare akajua kuwa yale maji ndio tatizo. Kwa hiyo kwa haraka Nyani akatengeneza vimfereji vya kutoa yale maji ili Kambare aishi kwa uhuru bila maji. Baada ya maji kuisha, Yule Kambare naye akafa.

Mambo ya kujifunza:

Yule Nyani angetafuta kuelewa kuwa Kambare anahitaji maji mengi ili aishi angeongeza maji kwenye bwawa badala ya kuyaondoa.

Kuna watu kwenye vikundi wana tabia kama za yule Nyani kwamba bila kujua wanaua vikundi badala ya kutafuta kuelewa kwanza vyanzo vya matatizo ya vikundi wao wanaondoa maji ya uhai wa vikundi na kuviacha vikifa.

9.      Kuepuka Tabia za Wanyama Zenye Kuua Umoja kwenye Kikundi

1.    Bata:            Kujivuta vuta mambo, kufanya kazi polepole na kuendekeza uvivu mapaka mambo ya kikundi yanazorota au kufa kabisa
2.    Bundi: Mtu anayefikiria ana akili kuliko wote kwenye kikundi- hutumia lugha ngumu kueleweka
3.    Chura:         Rudia rudia kitu kile kile mapaka anawachosha wenzake kundini
4.    Kenge:         Hatumii akili sawasawa, ujinga mwingi na kufanya maamuzi ya ovyo yenye kuwakatisha tamaa wenzake
5.    Kiboko:  Kulala lala na kupiga miayo, wakati wenzake wanachacharika, yeye ni kukaa tu hafanyi kazi.
6.    Kifaru:  Yeye hushambulia wengine kwenye kikundi bila sababu
7.    Kinyonga:    Kigeugeu, akiwa kwa mwanakikundi huyu anasema hili na akiwa kwa mwingine anasema tofauti hadi kuwagonganisha wanakikundi.
8.    Kobe:             Hujitoa akiudhiwa, hana uvumilivu kwenye changamoto zinazoikabili kikundi
9.    Kuku: Kuvuruga palipotengenezwa, kwenda tofauti na maono ya kikundi kwa kujali na kuzingatia mambo ya muda mfupi tu
10.  Mbuni:  Huficha kichwa na hufikiri hakuna shida kwenye kikundi hata kama zipo shida nyingi
11.  Nyati:           Kujihami tu kwa sababu ya woga, hakosolewi, ukimgusa tu anaazisha vita vya maneno au kupigana
12.  Nyoka:         Anajificha huku akiuma na kuchonganisha bila kusema.
13.  Nyumbu:      Woga wa kupindukia na kutotumia akili kabisa
14.  Paka:  Yeye anataka ahurumiwe tu na wenzake, hana mchango wowote kwenye kikundi ni mbinafsi sana
15.  Panya:        Hachangii chochote yeye hujificha tu na kujitokeza wakati wa neema
16.  Popo:  Hana msimamo, Kwa wanaokubali hoja yupo na kwa wanaopinga hoja yupo. Haeleweki
17.  Punda:  Wagumu kubadilika hata umuelimishe kwa namna gani misimamo yake ni yale yale ya zamani
18.  Samaki:  Hachangii hajibu, kazi kuteleza, kukwepa na kutoweka tu na huonekana hali ikitulia na kuwa shwari.
19.  Simba:  Hupigana na kuanzisha fujo kama hakubaliwi mawazo yake na wanakikundi
20.  Sungura:      Hukimbia kama kuna dalili za hatari na kwenda kinyume na makubaliano ya kikundi
21.  Tausi:          Yeye huringisha wengine na mambo mazuri aliyonayo ambayo wanakikundi wenzake hawana
22.  Tembo:         Hufunga njia bila sababu watu wasipite. Huzuia mawazo, maamuzi ya kikundi yasifanikiwe bila sababu
23.  Tumbili:       Mtu wa mizaha mizaha tu wakati wote hayuko makini hata kwa mambo muhimu ya kikundi
24.  Twiga:  Hujivunia elimu na ufahamu aliyonayo ambayo wanakikundi wenzake hawana na kwa hiyo kutotoa ushirikiano na wenzake. Mtu mjuaji sana

 10. Kufanya Tathmini na Maboresho ya Mahusiano Kila Baada ya Mwaka

Tathmini ya mahusiano ya kikundi ni vyema ikafanywa kila baada ya mwaka mmoja kwenye maeneo manne muhimu ili kupata fursa ya kufanyia maboresho.

Maeneo hayo ni

  1. Mfumo wa mawasiliano, utunzaji na utoaji wa taarifa
  2. Katiba
  3. Sheria ndogo ndogo za Kikundi
  4. Utendaji wa Uongozi

Mfumo wa mawasiliano, utunzaji na utoaji wa taarifa

Mawasiliano ndio uti wa mgongo wa mahusiano kwenye kikundi. Mfumo ukiwa mbaya, mahusiano yatakuwa mabaya. Ni lazima kikundi kikawa na sera ya habari na mawasiliano ambayo itakuwa ikiboreshwa kila mwaka

Sheria ndogo ndogo za Kikundi

Kila kikundi ni lazima ikawa na sera ya fedha na utawala. Sera hii itagusa pamopa na mambo mengine sheria za fedha, kukopa, faida, adhabu za kutowajibika na mikopo, wanachama wapya nk yafanyiwe tathmini na kama haiendani na wakati yaboreshwe ili kusaidia kikundi kukua. Ni vyema pia kuweka sera mbalimbali kulingana na uhitaji hasa zile zenye kulenga kuimarisha mahusiano kwenye kikundi.

Utendaji wa Uongozi

Tathmini ya uongozi ni ili kujua kama viongozi waliwajibika kama viongozi kwa wao wenyewe, kikundi na mwana kikundi moja moja.

Tathmini ni lazima ifanywe kwa kuzingatia viashiria vya utendaji wao (Key Performance Indicators) vilivyowekwa wakati wanakabidhiwa madaraka. Pia tathmini ifanywe ni kwa kiwango gani viongozi walifuata au kuvunja Katiba.

Matokeo ya Tathmini

Matokeo ya tathmini yatumike kuyafanyia maboresho yale maeneo yote yaliyoonekana kuzorota. Wakati wa kufanya maboresho ndio fursa pia ya kubadilisha uongozi wa kikundi pale itakapobidi na kama katiba inavyoelekeza. Maboresho mengine yanaweza kulazimisha mpaka Katiba ikaboreshwa na sheria pamoja na kaunini mbalimbali ili kukidhi mahitaji ya jumla ya maboresho.

Mwisho (End):

Kama umependa makala hii weka maoni yako ya shukrani hapo chini au washirikishe marafiki zako wa kwenye Facebook, Instagram, Linkedin, Whatsapp, Twitter na kwenye email au mitandao mingine ya kijamii. Wasiliana nasi kama unataka kuweka kwenye blogu au website yako kwa maelekezo zaidi

If you found this article helpful please leave the comment below or share to your friends in Facebook, Instagram, Linkedin, Whatsapp, Twitter and in email or other social media. Contact us if you plan to list in your blog or website for further instructions.

Tutembelee kwenye mitandao ya kijamii hapa chini:

We offer but not limited to the following:
Business Office Documents Development, Company Registration, Business Plan Development, Curricula Development for colleges, Office Digitization Consultancy, Online Presence and Marketing Consultancy, Leadership and Management Consultancy, Constitution Development  and much more

English Form

Fomu ya Kiswahili


city, country
mji, nchi